Saturday, July 28, 2012

NAMNA YA KUANZISHA BIASHARA.....

Ukitaka kufanya biashara yoyote ile unatakiwa kufanya utafiti. Kutokufanya utafiti ni chanzo cha biashara nyingi kuharibika. Lazima ujiulize kwamba unataka kufanya biashara gani? Usiseme unataka kufanya biashara yoyote ile kwani kusema kwamba unataka kufanya biashara yoyote ile ni kupoteza mwelekeo kwa kuwa utakuwa hujui unataka kufanya nini. Kama hujui cha kufanya hakuna kitu utakachokifanya. Hili ni tatizo la watu wengi. Hata baadhi ya watu niliokutana nao wakitaka ushauri wamekuwa wakisumbuliwa na tatizo hili. Njia ya kukusaidia kuamua ufanye biashara gani ni kwa kujiuliza umewahi kufanya kazi au biashara gani? Umesomea nini? Vipaji vyako ni vipi? Ni biashara ipi au kazi ipi unapenda zaidi kuliko nyingine na kwa sababu gani? Ukisha jiuliza maswali haya chukua kalamu na karatasi uandike maswali yako na kuyajibu. Ukikagua maswali na majibu yako utagundua shughuli unayoipenda, unayoiweza na una kipaji nayo na hiyo ndiyo inayokufaa. Ukishachagua biashara unayoipenda ni rahisi sana kufanikiwa kwani shughuli utazifanya kwa hiyari bila kujilazimisha. Kama unashindwa kuamua ni biashara gani ufanye, soma sura ya sita katika kitabu hiki. Nimeelezea kuhusu mawazo yanayoweza kukusaidia kuanzisha biashara mbalimbali ambazo unaweza kuzifanya. Kama utakuwa bado hujafikia uamuzi baada ya hapo basi tafuta na wasiliana na washauri ili mbadilishane mawazo na ufundishwe jinsi ya kuamua ufanye biashara gani.
Mambo mengine unayotakiwa kuyafanyia utafiti ni:-
(i) Kujua siri ya bishara unayotaka kufanya ili upate mbinu za kupata mafanikio. Unaweza kupata siri au kujifunza mbinu kutoka kwa watu wanaofanya biashara kama unayotaka kufanya. Suala hili ni gumu sana kwani wafanyabiashara wengi huwa wanaficha siri za biashara zao ili kulinda wasizidiwe maarifa na washindani wao. Unaweza kuipata siri hiyo kama utakwenda kupata ushauri toka kwa mfanyabiashara ambaye yuko mbali na mahali unapofanyia biashara, au tafuta ushauri kwa wataalamu wa mambo ya biashara.
(ii) Fanya utafiti wa soko la bidhaa unazouza au unazotarajia kuuza. Jiulize, je bidhaa unazotaka kuziuza zina soko? Utawauzia watu gani na utauzaje? Kama wewe ni mzalishaji, una mazao / bidhaa unapaswa kuuza kwa jumla, mchanganyiko ama rejareja? Je utatangaza vipi bidhaa zako? Maelezo ya namna ya kutangaza bidhaa zako utayapata katika Sehemu ya Tatu ya Kitabu hiki. Utafiti wa soko unaweza kuufanya kwa kuwauliza wafanya biashara waliotangulia maswali hayo ya utafiti kwani wao wamekuwapo kwenye soko na wanazijua siri za soko.
(iii) Tengeneza bajeti yako kwa kuorodhesha vitu vinavyohitajika na gharama zake ili kuweza kuanzisha biashara yako. Vitu hivyo ni:-
(a) Gharama za Kujenga au kupanga ofisi
(b) Gharama za Leseni ya biashara
(c) Makadirio ya kodi toka TRA
(d) Garama ya vifaa vya ofisi yaani, Samani, makaratasi, mitambo, mashine, nk
(e) Manunuzi ya malighafi au bidhaa za kuanzia biashara
(f) Idadi ya wafanyakazi na gharama za mishahara yao.
(g) Gharama nyinginezo kama vile, umeme, maji, nk.
(iv) Unatakiwa kujua ni mtaji kiasi gani unahitajika kuanzisha biashara yako. Mtaji huo utaujua baada ya kujumlisha gharama zilizoorodheshwa katika kupengele namba (iii)Gharama hizi ni za mwaka ule wa kwanza wa kuanzia
(v) Tafuta Mtaji.
Mtaji unaweza kupatikana kutoka kwenye vyanzo vifuatavyo:-
(a) Akiba au mshahara
(b) Msaada au mkopo kutoka kwa ndugu na jamaa.
(c) Kuingia ubia na mtu mwenye mtaji
(d) Mkopo toka baadhi ya asasi kama vyama vya akiba na mikopo (SACCOS), NGO za kifedha sipokuwa Benki kwani hizi huwa hazitoi mikopo kwa mtu anayeanzisha biashara.

TARATIBU ZA KISHERIA ZA KUFUATA ILI KUANZISHA BIASHARA

Baada ya kufanya utafiti na kupanga mipango ya kuanzisha biashara unatakiwa kwanza kuangalia taratibu za kisheria ambazo unatakiwa kuzifuata na kuzitekeleza. Kama biashara yako ni ndogo anza kama mtu binafsi. Faida ya kuanza biashara kama mtu binafsi ni urahisi wa kuanzisha biashara; urahisi na wepesi wa kutoa maamuzi kwani huhitaji ridhaa ya mtu mwingine kabla ya kutoa uamuzi; mtaji unaohitajika utakuwa mdogo kutokana na gharama za uendeshaji kuwa ndogo, biashara hii inaweza kuendeshwa kwa msaada wa familia kwa kumtumia mke au mume, watoto au ndugu na jamaa na raslimali za familia kama nyumba na samani. Unapoanzisha biashara na kuiendesha mwenyewe unakuwa huru tofauti na mifumo mingine. Matatizo ya kufanya biashara kama mtu binafsi ni:- Kushindwa kupanua biashara yako kwa ufinyu wa mtaji; kufilisiwa mali zako za binafsi iwapo biashara yako itafilisika kwani katika mfumo huu mali ya biashara na mali binafsi si rahisi kuzitenganisha; Kuongeza mtaji inakuwa ni vigumu, hivyo unaweza kushindwa kupanua biashara yako. Ili kuepukana na matatizo niliyoyataja hapo juu unaweza kuungana na watu wengine kufanya biashara kwa ubia. Faida za kufanya biashara kwa ubia ni: Kupata fursa ya kuongeza mtaji kwa kushirikiana na wafanyabiashara wengine ambao wataleta mitaji yao; Kuongeza ujuzi katika shughuli kwa kuleta wataalamu pale taaluma Fulani inapohitajika. Matatizo ya kuendesha biashara kwa njia ya ubia ni: Kufilisiwa mali zako binafsi endapo biashara yako itafilisika; kudhulumiana mali endapo moja wa wabia atakuwa si mwaminifu ambapo anaweza kuingia mikataba mibovu na kusababisha hasara ambayo itabebwa na wabia wote. Ni muhimu kuwachunguza watu tunaotaka kujiunga nao ili tujue kama ni waaminifu. Pia ni vyema kuwapo na mkataba wa maandishi mnapoanzisha biashara ya ubia mkimshirikisha mwanasheria kama shahidi ili kujikinga na kudhulumiana; Kufariki kwa mbia mmoja kunaweza kusababisha kuvunjika kwa ubia; kotokuelewana kwa wabia kunaweza kusababisha kuvunjika kwa ubia. Kama biashara ikikua unaweza kuanzisha kampuni. Mfumo wa uendeshaji wa kampuni unazo faida zifuatazo: unatenganisha majukumu ya wamiliki mali na kampuni yaani kampuni inaposajiliwa inakuwa inakuwa na hadhi na kutambulika kisheria kama ni mfumo tofauti na wamiliki. Mfumo huu unatenganisha majukumu kati ya menejimenti na wamiliki wa kampuni; madeni ya kampuni yatalipwa hadi kufikia kikomo cha mtaji uliowekezwa na wamiliki. Hivyo, mali binafsi za wamiliki wa kampuni haziwezi kukamatwa kufidia madeni ya kampuni endapo kampuni itafilisika. Mfumo wa kampuni unatoa nafasi ya kupanua mtaji kwa kukusanya mitaji kwa kuongeza wanahisa au kupitia soko la mitaji ya hisa. Mfumo huu ndiyo unafaa kwa biashara kubwa kwani unatoa nafasi ya kupanuka kwa biashara na kuendelea kuwapo kwa biashara hata kama baadhi ya wamiliki wake wakifa au kujitoa katika kampuni.

Mambo ya muhimu ya kutekeleza kisheria kabla ya kuanzisha biashara ni:-


(a) Kuwa na ofisi
(b) Kukata leseni
(c) Kusajiliwa na TRA kama mlipokodi na kupewa namba ya mlipakodi
(d) Kufanyiwa makadirio ya kodi ya mapato ya awali
(e) Kutimiza masharti mengine ya keshiria kuwa mfano kama wewe unataka kufanya biashara ya ukandarasi wa ujenzi wa majengo lazima usajiliwe kwenye Bodi ya Wakandarasi.

Kama unafanya biashara ya kati au kubwa unapaswa kufuata sheria. Ni makosa kufanya biashara bila kufuata sheria za nchi. Hata hivyo, kuna biashara zingine ndogo ndogo sana kiasi kwamba uanzishaji wake si rahisi kufuata sheria hizo hapo juu, mfano uuzaji wa maandazi, karanga na vitu vingine vidogovidogo. Hizi zinaitwa biashara zisizo rasmi au biashara ndogondogo. Ni vyema ukachunguza kama biashara unayoifanya ni ndogo au kubwa ili ujue kama unapaswa kufuata taratibu za kisheria au la, kwani kutokujua utaratibu na sheria siyo kinga ya kukufanya usishitakiwe.



5 comments:

  1. Ahsanteni sna kwa ushauri huu na naamini utanisaidia katika kuombaanzisha biashara yangu.Naomba mkitou ushauri tena kuhusu biashara mnitaarifu.

    ReplyDelete
  2. Ahsanteni sna kwa ushauri huu na naamini utanisaidia katika kuombaanzisha biashara yangu.Naomba mkitou ushauri tena kuhusu biashara mnitaarifu.

    ReplyDelete
  3. amani kwenu wataalamu wangu.. mmefumbua akili za watanzania wengi hii ndio imani yangu

    ReplyDelete